Jumanne , 9th Feb , 2021

Kampuni ya michezo ya kubashiri Tanzania MERIDIAN BET imejitokeza kumsaidia Kijana Shabani Salum (34) Mkazi wa Chanika Jijini Dar es salaam aliyekuwa mchibaji wa madini baada kupata ugonjwa ambao bado haujajulikana hali iliyosababisha kulala kitandani kwa zaidi ya miaka 10.

Pichani Kijana Shabani Salum (34) Mkazi wa Chanika Jijini Dar es salaam aliyekuwa mchibaji wa madini baada kupata ugonjwa ambao bado haujajulikana.

Awali akielezea chanzo cha tatizo hilo Shabani anasema alianza kupata maumivu ya bega akaenda hospitali akiwa mzima aliporudi akapanda kitandani kwa ajili ya kupumzika tangu siku hiyo hajawai kuinuka tena ikiwa ni miaka 10 mpaka sasa.

"Siku moja nikiwa nyumbani nilisikia maumivu ya bega nikaenda hospitali kwa ajili ya kupata dawa ya kuchua nikapewa, niliporudi nyumbani nikawa na uchovu nikaingia chumbani kupumzika nilipolala sikuweza kuinuka tena tangu mwaka 2011 hadi leo badala yake miguu ikaanza kujikunja na kuwa midogo sana huku ikiuma mno, napata maumivu makali sana usiku silali tumbo linajaa maji" amesema

Akizungumza wakati akitoa msaada wa Vyakula na Fedha Kiasi cha Shilingi laki sita (600000) Meneja Ustawi Kampuni ya Meridian Bet, Amani Maeda amesema kampuni hiyo imekuwa ikitoa msaada kwa jamii zenye uhitaji mara kwa mara na hivyo wakaguswa na matatizo anayoyapitia Shabani na familia yake kwa sasa sambamba na kuahidi kuendelea kuisaidia familia hiyo zaidi.

"kampuni yetu imekuwa ikisaidia jamii zenye uhitaji mara kwa mara kama sehemu ya kurudisha kwa jamii kwa namna inavyotuunga mkono na kiukweli tumeguswa sana na matatizo anayoyapitia kijana huyu na familia yake hivyo tumewaletea vyakula na fedha shilingi 600000 na tutaendelea kushirikiana nao kwa ukaribu zaidi." amesema

Kwa upande wake Shabani Salum ameishukuru Kampuni ya Meridian Bet kwa msaada huo kwani utasaidia katika maisha yao ya kila siku yeye pamoja na familia yake

Nao Wazazi wa Shabani mbali ya kuishukuru Kampuni hiyo wamesema fedha hizo zitawasaidia kuwaendeleza kiuchumi kwani awali walikuwa na biashara ya sabuni lakini ilikufa kutokana na mtaji kutumika kumuuguzia kijana wao aliyeugua kwa muda mrefu.

Kampuni ya michezo ya kubashiri Tanzania MERIDIAN BET imetoa Unga wa Ugali, Unga wa Ngano, Sabuni ya Unga, Sukari, Mchele, na Mafuta ya kupikia pamoja na fedha kiasi cha shilingi laki sita.