Jumatatu , 11th Sep , 2017

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewapongeza wastaafu wa Mahakama kwa kuwa na busara na weledi, huku akionesha kushangazwa na viongozi wengine ambao wanasema sema baada ya kustaafu.

Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli

Akizungumza mapema leo mara baada ya kumuapisha Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Prof: Ibrahim Juma, Ikulu jijini Dar es salaam, Rais Magufuli amesema wazee hao wengine ambao wamestaafu hawachoki kusema, huku akiwafananisha na watu wanaowashwa na kitu.

“Waheshimiwa Majaji hawa ni waadilifu sana, huwezi ukamsikia jaji Chande anazungumza chochote, huwezi ukamsikia Jaji mstaafu Samatta anazungumza chochote, hawa majaji walioko hapa ukiangalia na wastaafu wengine wa maeneo mengine, hawachoki kusema, wana washwa washwa", amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli ameendelea kwa kusema "ndiyo maana mimi nawapongeza sana mahakama ni safi mno, nina hakika wao wakitaka kutoa ushauri wowote ule lazima watakuwa wanaku-consult na wanakueleza, ndiyo faida ya kujua sheria”, amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli leo amemuapisha Prof. Ibrahim Juma kuwa Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kumteua jana kushika wadhifa huo.