Jumapili , 11th Apr , 2021

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewahakikishia Watanzania kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan itaendelea kutoa fedha za kugharamia mradi wa umeme wa maji ya Mto Rufiji (RHPP) ili ukamilike kwa wakati.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipotembelea mradi wa umeme wa maji ya Mto Rufiji (RHPP)

Aliyasema hayo Jumamosi, Aprili 10, 2021, baada ya kukagua mwenendo wa mradi huo unatarajiwa kukamilika June 2022. Amesema kuwa Serikali itahakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyostahili.

”Lengo la kuanzisha mradi huu ni moja ya juhudi za Serikali za kupunguza gharama za umeme kwa wananchi kwa sababu uzalishaji wake ni wa gharama nafuu ukilinganisha na vyanzo vingine. Uniti moja ya umeme unaozalishwa kwa kutumia maji inagharimu shilingi 36 hadi shilingi 50 huku umeme unaotumia vyanzo vya mafuta uniti moja inazalishwa kwa gharama ya shilingi 440 hadi shilingi 600,” alisema Waziri Mkuu.

Aidha Waziri Mkuu alifarijika kuona kazi nzuri yenye viwango na ubora wa hali ya juu inayofanywa na Kampuni ya Arab Contractors kwa pamoja na ile ya Elsewedy  Electric zote kutoka nchini Misri chini ya usimamizi wa TANESCO, TANROADS na Wizara ya Nishati.

Aliongeza kuwa bwawa hilo linatarajiwa kuzalisha megawati 2,115 ambazo zikijumlishwa na megawati 1,500 zinazozalishwa na vyanzo mbalimbali nchini hivi sasa zitaifanya Tanzania kuwa na umeme utakaotosheleza mahitaji yake na ziada kuuzwa kwa majirani hivyo mradi huo utawawezesha Watanzania kupata umeme mwingi na wa gharama nafuu.