Ijumaa , 30th Jan , 2015

Bunge limechachamaa na kutaka serikali ianze kuchukua hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwakamata, kuwashtaki na kuwafilisi wale wote wanaohusika katika ubadhirifu na upotevu wa fedha za serikali kutokana na kukosa uzalendo na uwajibikaji

Mbunge wa Viti Maalum Ester Bulaya

Bunge limechachamaa na kutaka serikali ianze kuchukua hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwakamata, kuwashtaki na kuwafilisi wale wote wanaohusika katika ubadhirifu na upotevu wa fedha za serikali kutokana na kukosa uzalendo na uwajibikaji badala ya kila mwaka bunge kupokea ripoti ya ubadhirifu unaolisababishia taifa hasara ya mabilioni ya shilingi.

Baadhi ya wabunge pia wamesema kwamba kujiuzulu ama kufukuzwa kazi pekee si suluhisho ili kuwa na taifa lenye nidhamu katika matumizi ya fedha za umma.

Bunge limepata fursa ya kuzijadili taarifa za kamati ya bunge ya hesabu za serikali ambayo taarifa yake inaonesha kuwa zaidi ya shilingi bilioni 100 zimekwepwa kulipwa na makampuni mbalimbali kwa kivuli cha misamaha ya kodi.

Pia taarifa inaonesha kuwa takribani bilioni 8 zimepotea baada ya mamlaka ya bandari kufanya manunuzi ya dharura bila kibali cha mlipaji mkuu wa serikali jambo liliwafanya baadhi ya wabunge kugeuka mbogo.

Hata hivyo wakati majadiliano yakiendelea kukaibuka mabishano ya kisheria dhidi ya Tundu Lissu na Mwanasheria mkuu wa serikali George Mcheche Masaju baada Lissu kutaka Rais awawajibishe baadhi ya majaji waliohusika katika sakata la Tegeta Escrow kwa kuwa katiba inampa mamlaka.

Kutokana na kauli hiyo Masaju akaliambia bunge kuwa tume ya utumishi wa mahakama kwa mujibu wa katiba ndiyo inapaswa kumshauri Rais juu ya masuala ya nidhamu za majaji.
 
Kutokana na kile kinachodaiwa kuwa ni kuepuka kuingilia mihimili mingine hasa mahakama baaadhi ya wabunge wameonesha kutoridhika na hoja hiyo kutokana na wabunge kuzuiwa kulijadili sakata la UDA kutokana na taarifa za uwepo wa kesi kadha wa kadha mahakamani zinazohusu UDA.

Hiyo imetokana na mwanasheria mkuu wa serikali kushauri kutojadiliwa bungeni kutokana na kamati ya bunge ya hesabu za serikali za mitaa kuitaka serikali kutoa maelezo bungeni endapo ni kweli hisa za UDA zimeuzwa kwa kampuni binafsi ya Simon Group Limited au la.
 
Mara baada ya muongozo huo mwenyekiti Mh Musa Azan Zungu akaitaka kamati uongozi ya bunge kukutana ili kulijadili suala hilo kwa madai kuwa kuna mambo yako mahakamani na mengine hayapo mahakamani lakini bunge linakosa fursa ya kuyajadili.