Jumanne , 19th Apr , 2016

Chama Cha Mapinduzi wilaya ya Arusha Mjini kimepata ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa wenyeviti wa serikali ya mtaa kwa kupata viti vitano na CHADEMA vitatu.

Katibu wa CCM wilaya ya Arusha mjini Feruzi Bano,

Uchaguzi huo ulifanyika kutokana na wenyeviti wa mitaa tisa kuhamia katika vyama mbalimbali vya siasa wakati wa uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka jana.

Akizungumza na East Africa Radio ofisini kwake, Katibu wa CCM wilaya ya Arusha mjini Feruzi Bano, amesema ushindi huo unatokana na kasi ya Rais Dk John Magufuli ya utumbuaji majipu ambayo imewakuna wananchi wengi na kuanza kuipenda CCM

Bano ametaja mitaa ambayo CCM imeshinda ni pamoja na mtaa wa Olamuriaki katika kata ya Sombetini na mtaa wa Shangarau kaya ya Moivaro ambapo katika mitaa yote hiyo CCM imepita bila kupingwa baada ya CHADEMA kushindwa kusimamisha wagombea.

Ametaja mitaa mingine ambayo CCM imeshinda ni pamoja na mtaa wa Makao mapya kata ya Sinoni,mtaa wa Bondeni kata ya Kati,mtaa wa Kilimaji kata ya Moshono.

Kwa upande wa wajumbe wa serikali za mitaa amesema CCM ilipata ushindi wa kishindo kwa kupata wajumbe watatu huku CHADEMA ikiambulia mjumbe mmoja.

Kwa mujibu wa Bano CCM ilishindwa kushinda katika mitaa hiyo mitatu kutokana na mvua kubwa iliyokuwa inayesha jijini hapa juzi hali iliyosababisha wana CCM wenye umri mkubwa kushindwa kwenda kupiga kura

Ameongeza sababu nyingine kuwa ni karatasi za kupigia kura kutokuwa na muhuri wa Halmashauri ya Jiji pamoja na kutukuwa na vitambulisho vya kuonyesha kama kweli waliopiga kura katika mitaa hiyo walikuwa wakazi husika.

Katika uchaguzi huo kwenye kata ya Daraja mbili mtaa Sanare CCM na CHADEMA wagombea wa nafasi ya uenyekiti wa serikali ya mtaa walifungana hivyo uchaguzi huo utarudiwa tena baada ya msimamizi wa uchaguzi ambaye pia ni mkurugenzi wa Jiji Juma Iddy kutangaza tarehe nyingine ya uchaguzi.