Jumatatu , 18th Sep , 2017

Katibu wa Mbunge wa Tarime Vijijini John Heche, amefunguka na kusema wanamshukuru Mungu dereva wa mbunge wao aliyejeruhiwa mwishoni mwa wiki iliyopita hajapata madhara makubwa katika fuvu la kichwa na amepata ruhusa ya kurudi nyumbani.

Katibu Zabloni Mrimi ambaye pia alikuwa mmoja wa waangalizi wa usalama wa dereva wa Heche tangu alipopata ajali ya kushambuliwa kwa mapanga amesema hali ya mgonjwa imebadilika na kuwa yenye kuridhisha na kutia moyo.

"Baada ya matibabu aliyokuwa akipatiwa hospitali ya Bomani tulimpeleka hospitali nyingine kwa ajili ya vipimo vya 'X Ray' na uchunguzi mwingine zaidi, Lakini jambo la kumshukuru Mungu pamoja na kwamba alipata majeraha sehemu mbaya ila imeonekana kuwa fuvu lake la kichwa halijapata madhara"

Pamoja na hayo ameongeza kuwa taarifa walizopata kutoka kwenye jeshi la polisi ni kwamba bado wanaendelea na msako wa kuwakamata waliohusika na tukio hilo ikiwa ni pamoja na kusikia kauli ya Kamanda wa Polisi kuwataka waliofanya shambulio hilo waweze kurudisha mali za dereva huyo.