Ijumaa , 18th Aug , 2017

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amewataka Makamishna wastaafu wa Polisi kuendeleza elimu ya Polisi Jamii pamoja na kutoa msaada katika jeshi la Polisi pindi wanapokuwa katika maisha ya uraia ili kuhakikisha wahalifu hawapati nafasi.

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro.

IGP Sirro ameeleza hayo wakati wa sherehe zilizoambatana na Gwaride maalumu la kuwaaga Makamishna wastaafu wa Polisi Paul Chagonja, Hamdan Omar Makame na Kenneth Kaseke lililofanyika katika viwanja vya Chuo cha Maafisa wa Polisi jijini Dar es Salaam ambapo wastaafu hao walisukumwa kwenye gari maalumu na Makamishna Wasaidizi Waandamizi sita ikiwa ni utaratibu wa Jeshi hilo katika kuwaaga maofisa wakuu.

“Upolisi ni taaluma kama zilivyo taaluma nyingine hivyo utaalamu hauzeeki na kwetu sisi tunaondelea kubaki Jeshini tutaendelea kufuata yale yote mazuri mliyofanya na nyie mnapokuwa nje ya utumishi endeleeni kutusaidia kwa mawazo na milango yetu ipo wazi ili kuhakikisha nchi inaendelea kuwa salama” Alisema IGP Sirro.

Katika hatua nyingine, Kamishna Paul Chagonja akizungumza baada ya kuagwa rasmi ambaye alikuwa Kamishna wa Oparesheni na mafunzo kwa muda mrefu amewaasa Maofisa na askari kuendeleza tamaduni na maadili ya Polisi pamoja na kufanya kazi kwa weledi pamoja na nidhamu kwa kuwa ndiyo msingi wa askari Polisi popote pale wafanyapo kazi zao hivyo amewaomba kuendelea kusimamia sheria bila ya kumuonea mhalifu yeyote.