Jumatatu , 20th Nov , 2017

Serikali ya Kenya imeitumia barua serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikitaka ufafanuzi kuhusu suala la vifaranga vilivyoteketezwa hivi karibuni ambavyo vinadaiwa kuingizwa nchini kutokea Kenya.

Taarifa ya serikali kupitia wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imetibitisha kupokea barua hiyo huku serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiahidi kuijibu na kuitolea ufafanuzi kama ilivyofanya mwanzo.

“Vile vile serikali imepokea barua kutoka Serikali ya Kenya kuhusu masuala haya, na Serikali itaijibu barua hiyo kutoa ufafanuzi”, imeeleza sehemu ya taarifa ya wizara juu ya ufafauzi kuhusu suala la vifaranga pamoja na mifugo iliyoingizwa nchini bila kufuata sheria.

Aidha serikali ya Tanzania imesema itaendelea kuhakikisha inafuata sheria zote bila kuathiri uhusiano wake na nchi zingine, huku ikizitaka nchi zote duniani, ikiwemo Kenya, kufuata miongozo ya WTO na Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE) kwa kutoa vibali (export permit) kwa mtu yeyote anayetaka kusafirisha mifugo nje ya nchi.

Kabla ya kuteketezwa kwa Vifaranga hivyo serikali imesema Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo Tanzania alimpigia simu Mkurugenzi wa Huduma za Mifugo wa Kenya kutaka kujua kama Mamlaka za Kenya zina habari kuhusu vifaranga hivyo ili virudishwe lakini alisema hana taarifa kuhusu vifaranga hivyo na kwamba Kenya haiko tayari kuruhusu vifaranga hivyo kurudishwa nchini mwao.