Alhamisi , 27th Jul , 2017

Mbunge wa jimbo la Nzega Vijijini ambaye pia ni Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Dk. Hamisi Kigwangalla amekabidhi gari maalum la kubebea wagonjwa (Ambulance) mpya na la kisasa katika Kituo cha Afya Busondo

 kilichopo Tarafa ya Puge ambalo litakuwa msaada mkubwa kwa wananchi wa Nzega Vijijini.

Tukio hilo la kukabidhi gari hilo limefanywa na Mkuu wa Wilaya ya Nzega, mkoani  Tabora, Mh. Geofrey Ngupula ambaye alitoa agizo kali kwa Mganga Mkuu wa Kituo hicho kuhakikisha gari hilo linatumika kwa shughuli zilizokusudiwa ikiwemo za kubebea wagonjwa na akina mama wajawazito kuwawaisha sehemu muhimu za kutolea huduma stahiki.

"Gari hilo lipatikane kituoni  wakati wote pamoja na dereva, tumeshahakikishiwa hapa Halmshauri imesema ina mafuta ya kutosha litakuwa linajazwa lita 90, kila yatakapokuwa yametumika hivyo kusiwe na kisingizio kingine cha kuweza kudai mafuta ama kuwatoza wananchi gharama na atakayefanya hivyo serikali hii si ya mchezo hatua kali zitafuata, tutakutumbua tu. Gari hili la kisasa litunzwe na kulindwa ili liweze kutumika kwa miaka mingi ijayo na kuwa msaada kwa tarafa hii na wananchi wote watakaopata msaada", amesema Ngupula.

 Mkuu wa Wilaya ya Nzega, mkoani  Tabora, Mh. Geofrey Ngupula akizungumza mara baada ya kuzindua rasmi gari jipya na la kisasa la kubebea wagonjwa lililokabidhiwa katika kituo cha Afya Busondo, Tarafa ya Puge.

Kwa upande wake, Dk. Kigwangalla amewaomba wananchi waendelee kumuombea kwa kazi anayofanya ikiwemo jukumu la kulitumikia taifa katika nafasi yake ya Unaibu Uwaziri wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na kuishukuru serikali ya awamu tano ya Rais Magufuli kwa kuweza kuwa karibu na wananchi ikiwemo kushughulikia suala la maji kutoka Ziwa Victoria na kuelekea mkoa wa Tabora na wilaya ya Nzega na maeneo mengine.

"Rais wetu anatupenda na tuendelee kumuunga mkono hasa juhudi zake za kulinda rasilimali za nchi yetu na pia katika kushughulikia mafisadi na wahujumu uchumi wa taifa letu. Mimi Mbunge wenu pia muendelee kuniombea na kila siku mawazo yangu na akili yangu ipo pamoja nanyi ndiyo maana nimeweza kuwaletea gari hili la wagonjwa, na pia kufanikisha kuandaa kambi maalum ya matibabu bure ya wiki moja kwa wananchi wote wa Nzega bure", amesema Dk. Kigwangalla.

Kwa upande mwingine, tukio la ukabidhiwaji wa gari hilo liliweza kushuhudiwa na  viongozi mbalimbali wakiwemo Madiwani wa Jimbo hilo na wale wa jimbo jirani ikiwemo Bukuene, Viongozi wa ulinzi na Usalama pamoja na Mganga Mkuu wa Wilaya ya Nzega.