Jumanne , 21st Nov , 2017

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema amesema kwamba kisasi cha CCM kuchukua wanachama wake kitasaidia kuwaondoa wavulana kwenye mapambano ya siasa za upinzani.

Lema ameyasema hayo ikiwa ni muda mfupi baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana Chadema, Patrobas Katambi kuomba kuomba ridhaa ya kuingia ndani ya Chama cha Mapinduzi leo katika kikao cha halmashauri Taifa.

Lema amesema kwamba CCM imekuwa na kisasi kikubwa baada ya aliyekuwa Waziri wa Maliasili mstaafu na Mbunge wa Singida Kaskazini  Lazaro Nyalandu kuondoka CCM 

"Baada ya Lazaro kuondoka CCM , CCM wamekuwa na kisasi kikubwa , ambacho kimsingi kitasaidia kuondoa wavulana ktk mapambano haya , bado Mameya wawili ? Na kijana mwingine aliyekuwa shupavu 2010-2015. Msiogope kwani wanawaogopa sana na ndio sababu ya matendo haya" Lema.

Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Chama hicho Dr. Vicent Mashinji amesema kwamba "Ni muda wa kutofautisha kati ya wanaume na wavulana! wana CHADEMA msihofu tunazidi kuimarika. Kila abiria atashuka kwenye kituo chake lakini safari ya ukombozi inaendelea".

Hata hivyo juhudi za kumtafuta Lema kwa ajili ya kumtaja jina kijana huyo anayetarajiwa kuondoka Chadema hazijazaa matunda kwani simu ya Mbunge huyo haijapokelewa.