Jumamosi , 23rd Jul , 2016

Mwenyekiti mstaafu wa CCM Dkt Jakaya Kikwete, amekabidhi nafasi cha uenyekiti wa chama hicho kwa Dkt John Pombe Magufuli, huku akimtaka kushughulikia baadhi ya mapungufu yanayokitia hasara chama ikiwemo kuokoa mali za chama.

Dkt Jakaya Kikwete (Kushoto) akiteta jambo na Dkt Magufuli (Katikati) na Katibu Mkuu Abdulrahman Kinana (kulia)

Kikwete ambaye pia ni Rais Mstaafu wa Tanzania, ametoa hotuba yake ya mwisho kama mwenyekiti wa chama hicho leo katika mkutano mkuu maalum uliofanyika mjini Dodoma, na kutoa onyo kwa watu wote wanaoshikilia mali za chama kwa manufaa yao binafsi.

Akitaja baadhi ya mali hizo, Jakaya Kikwete amesema kuna wanachama ambao wamejimilikisha viwanja vya chama hicho bila utaratibu rasmi na kuwapa tahadhari ya kuvirejesha katika chama haraka.

Amemtaka mwenyekiti mpya mpya wa chama hicho kushughulikia suala la viwanja ambavyo bado havijapewa hati ili viendelezwe na kugeuzwa kuwa vitega uchumi na kuongeza wigo wa mapato ya chama.

“Mkoa wa Dar es salaam pekee una viwanja 279 lakini ni 45 pekee ndivyo vina hati angalau UVCCM wanajitahidi kujenga majengo ya vitega uchumi na kuna wazee wengine wa chama wameamua kujimilikisha viwanja vya chama, sisemi kwamba ni MAJIPU hapana, nawakumbusha ili viwanja hivyo viendelezwe, chama kipate mapato”

Aidha Kikwete amewakumbusha wakuu wa wilaya kuwa wanapaswa kutambua mojawapo ya jukumu walilonalo ni kulinda maslahi ya chama katika ngazi ya wilaya.

“Kuna wakuu wa wilaya wamesema eti wao ni wasomi na kwamba siasa haiwahusu, lakini wajue kuwa wao ni wajumbe wa kamati za siasa za wilaya, hivyo wajue kuwa wamewekwa kule kwa makusudi kama kiungo kati ya chama na serikali”

Amesisitiza kuwa ana imani kubwa kuwa Dkt Magufuli anatosha na ataweza kukisimamia vizuri chama hicho.