Jumatatu , 22nd Feb , 2016

Halmshauri ya Manispaa ya Kinondoni imekataa mpango wa mchango wa sh. Milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa kutoka kwa mawaziri, naibu mawaziri,makatibu wakuu na makamu wa Rais.

Meya wa Manispaa ya Kinondoni, Boniface Jacob.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam Meya wa Manispaa ya Kinondoni Boniface Jacob amesema kuwa halmshauri hiyo inajitosheleza na kwamba kuwaambia mawaziri watoe sehemu ya mshahara wao kusaidia manispaa hiyo ni kuwaonea.

Mhe. Jacob amesema kuwa Halmshauri ya Kinondoni ina wigo mpana wa kukusanya kodi lakini alichokibaini ni kwamba kumekuwepo na uzembe wa ukusanyaji kodi uliokuwa ukifanywa na baadhi ya watendaji wa halmashauri hiyo.

Amesema kuwa kuwa kuna mikataba mingi ambayo wamegundua iliingiwa kimakosa na kwamba hali hiyo imechangia halmashauri kupata hasara hivyo karibu asilimia 50 ya mapato yamekuwa yakipotea bila sababu za msingi.

Meya huyo kutoka chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), amesema kuwa kwa sasa lengo la manispaa hiyo ni kuhakikisha wanakusanya zaidi ya bilioni 100 kwa mwaka.