Jumatatu , 23rd Oct , 2017

Baada ya serikali kuandaa uchaguzi wa marudio kutokana na sababu mbalimbali, Diwani wa Kata ya Sombetini Arusha, Ally Bananga kupitia mtandao wa kijamii ametaka kujua  nani aliyewaloga watanzania kiasi cha kushindwa kufikiri gharama zinazotumika

kwenye uchaguzi huo zingesaidia kuboresha huduma za kijamii.

Bananga amedai kwamba Serikali inatenga fedha zingine milioni 200 kwa ajili ya uchaguzi wa marudio ikiwepo sehemu ambazo madiwani wamejiuzulu na kuhoji kwamba hivi diwani asingejiuzulu hizo fedha mil 200 kama zisingweza kununua madawa katika hospitali.

Kiongozi huyo amehoji,  "Hivi?? Watanzania nani aliyetuloga????? Siyo serikali siyo wananchi aiseeee!!! hivi Diwani asingejiuzulu hizo fedha mil 200 zisingenunua madawa hospitali? Je, zisingejenga matundu ya vyoo mashuleni? Je, zisingejenga vituo vya polisi maeneo yenye uhitaji? " Bananga

Bananga ameongeza "Kama Tanzania haikulogwa basi kuna taifa litakuwa lilitusomea alibadri siyo bure!!!!"  

Oktoba 4, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ilitangaza kwamba uchaguzi mdogo wa madiwani katika kata 43 Tanzania utafanyika Novemba 26 mwaka huu ambapo Mwenyekiti wa NEC  Jaji  Semistocles  Kaijage, alisema kuwa uchaguzi huo unafanyika kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo baadhi ya madiwani kufariki dunia, kujiuzulu, kutohudhuria vikao na wengine ushindi wao kutenguliwa na Mahakama.