Jumapili , 25th Dec , 2016

Serikali ya mkoa wa Dar es Salaam amewataka wananchi wote mkoani humo kuitumia Sikuu ya Krismasi kwa kuiombea Tanzania ili iendelee kuwa ya amani na utulivu.

Ally Hapi - DC Kinondoni

Akitoa salamu hizo kwa niaba ya serikali ya mkoa huo, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mkoa wa Dar es Salaam Ally Hapi amewasihi pia wananchi kuwaombea viongozi wa nchi akiwemo Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na wasaidizi wake wote ili waendelee kuitumikia nchi vema.

Pia amewataka kuwajali walemavu, yatima na watu wasiojiweza ili nao waweze kusherehekea siku hii kwa furaha. 

Katika taarifa yake, Hapi amezikumbusha familia kuchukua tahadhari za kiusalama katika siku hii ikiwemo kuongeza umakini na uangalizi wa watoto maeneo ya fukwe (beach) ili kuondoa uwezekano wa maafa, kutoondoka nyumbani bila kuacha angalau mtu mmoja mzima wa kubaki kutazama usalama wa nyumba na kuzidisha umakini katika matumizi ya barabara.

"Tusisite kutoa taarifa kwa jeshi letu la polisi pindi tunapoona viashiria vya uhalifu au kuvunjika amani katika maeneo tuliyopo". Amesema Hapi.