Ijumaa , 18th Aug , 2017

Rais wa chama cha Wanasheria Tanzania (TLS) na Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Tundu Lissu amefunguka kwa kuwataka wakuu wa vyombo vya usalama nchini wawaelekeze watumishi wao kazi za kufanya na siyo kupoteza muda na rasilimali za nchi.

Rais wa chama cha Wanasheria Tanzania (TLS) na Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Tundu Lissu.

Lissu amesema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano uliyoitishwa na CHADEMA wenye lengo la kuzungumzia namna nchi inavyoenda kufilisika na ndipo alipomtaka Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa, Dkt. Modestus Francis Kipilimba na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro kuwapa uweledi mzuri wa kufanya kazi vijana wao.

"Wale vijana wenu ambao mmekuwa mkiwatuma wanifuate kila nilipo kwa kipindi cha wiki tatu sasa, jana nimefanikiwa kuwakaba kanisani St. Peters. Hivyo wakubwa hawa wa vyombo vya usalama wawaelekeze watumishi wao namna ya kutumia muda na rasimali ya nchi hii", alisema Lissu.

Pamoja na hayo, Lissu ameendelea kwa kusema "Wafanye kazi ya kupambana na wahalifu na siyo kupoteza muda wao na pesa za walipa kodi kuhangaika na raia ambao wanatimiza uhuru wao wa kuiwajibisha serikali iliyoko madarakani".

Kwa upande mwingine, Lissu amemtaka Kamanda Sirro pamoja na Kamanda Kipilimba kupamba na wahalifu na wamuachie yeye kazi ya kuwajibisha waliyoko madarakani kwa mujibu wa sheria za nchi.