Jumatatu , 27th Feb , 2017

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imesema itamchukulia hatua muwekezaji aliyetoa ardhi kwa serikali ya mkoa wa dar es Salaam kwa ajili ya ujenzi wa viwanda, kwa madai kuwa ardhi aliyoitoa siyo yake.

Waziri William Lukuvi

Waziri wa wizara hiyo, William Lukuvi, ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam na kufafanua kuwa muwekezaji huyo aliidanganya serikali pamoja na kumdanganya mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda, ambaye ndiye aliyekabidhiwa eneo hilo kwa niaba ya serikali.

Mbali na kosa la kuidanganya serikali, Lukuvi pia amesema atamchukulia hatua mfanyabiashara huyo kwa kumiliki ardhi kinyume cha sheria.

Kuhusu Mkuu wa Mkoa , Paul Makonda, Lukuvi amesema tayari amekwishafanya naye mawasiliano na kumuelewesha kuwa alidanganywa kwa kuambiwa kuwa anapewa eneo kwa ajili ya viwanda, huku eneo lenyewe likiwa ni mali ya serikali.

Siku ya Jumanne wiki iliyopita Makonda alikabidhiwa ekari 1500 za ardhi na Mkurugenzi wa Azimio Housing Estate Mohamed Iqbal kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vidogo vigogo nchini, katika eneo la Kigamboni Dar es Salaam.

Akizungumza mara baada ya makabidhiano hayo eneo la Kisarawe II wilaya ya Kigamboni Mkurugenzi huyo alisema wameamua kumkabidhi eneo hilo ili kuunga mkono jitihada za Rais Magufuli za kuijenga Tanzania ya viwanda na kuwakomboa wananchi wenye uchumi wa kati.

Kwa upande wake Makonda aalieleza kuwa dhamira ya viwanda ya Rais Magufuli inabidi itafsiriwe kwa vitendo, hivyo eneo hilo litatumika kwa ajili ya ufugaji, kilimo, usindikaji, utengenezaji wa sabuni na eneo hilo litatumika na wilaya zote.