Jumatatu , 11th Sep , 2017

Waziri wa Ardhi nyumba na Maendeleo ya Makazi Mheshimiwa William Lukuvi ameagiza kuondolewa kwa wafugaji wanaochunga mifugo yao kwenye mashamba ya wakulima katika tarafa ya Idodi mkoani Iringa na kusababisha uharibifu wa mazao ya wakulima.

Waziri wa Ardhi nyumba na Maendeleo ya Makazi Mheshimiwa William Lukuvi.

Akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi gari la wagonjwa kwa kituo cha afya Idodi Waziri Lukuvi amesema hakuna sababu ya kuendelea kuishi na wafugaji hao huku akiwaonya viongozi wala rushwa wanaowaficha na kuwahifadhi wafugaji hao.

Mkuu wa mkoa wa Iringa Bibi Amina Masenza amewataka wananchi wa Idodi kutoa ushirikiano na kuwataja wafugaji wote ambao wamekuwa chanzo cha vurugu ili kuwaondoa wafugaji hao waliovamia kijiji na kusababisha mgogoro.

Katika mahojiano na baadhi ya wananchi wa eneo hilo wamesema wafugaji hao wanapata kiburi kutoka kwa baadhi ya watendaji wa serikali ambao wamekuwa wakiwakamata mara wanapofanya uhalifu na kuwaachia bila kuwashitaki.