Jumapili , 19th Mar , 2017

Umoja wa Madaktari, Wauguzi na Wataalamu wa Meno nchini Kenya,(KMPDU), umepinga vikali hatua ya Serikali ya Kenya kuleta madaktari kutoka Tanzania wakati Kenya ina madaktari wengi ambao hawaajiriwa.

Ouma Oluga (Kushoto)

Kupitia kwa Katibu Mkuu wa umoja huo, Ouma Oluga umepinga hatua hiyo na kudai kwamba, Serikali ya Kenya haijawa makini katika kushughulika na tatizo la upungufu wa madaktari nchini humo.

Akizungumza na mtandao wa The Star wa nchini Kenya Bw. Oluga amesema, hata hivyo, watawakaribisha madaktari kutoka Tanzania na kuwaunganisha katika umoja huo na kwamba watapaswa kupitia mitihani itakayoandaliwa na Bodi ya Wauguzi.

Amesema mitihani hiyo itachukua siyo chini ya miezi mitatu labda kama tu hitaji hilo halitaangaliwa.

Bw. Oluga amedai kwamba, Kenya ina zaidi ya madaktari 1,400 ambao wanasubiri ajira, hivo itakuwa, gharama kubwa na dalili ya kushindwa kutumia fedha za umma vizuri kwa kuwa na madaktari 500 wa Kitanzania kwa gharama ya Shilingi 20,000 kwa siku.

Mapema jana Rais wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alikubali na kuridhia ombi la Serikali ya Kenya na kuahidi kutuma madaktari 500 kusaidia kukabiliana na tatizo la upungufu wa madaktari nchini humo kufuatia mgomo wa madaktari ulioisha hivi karibuni baada ya kudumu kwa siku 100.