Alhamisi , 21st Sep , 2017

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kufungua mkutano wa mwaka wa Chama cha Majaji na Mahakimu wa nchi za Jumuiya ya Madola unaofanyika nchini kwa mara ya kwanza kuanzia Septemba 24 hadi 28 mwaka huu.

Hilo limethibitishwa leo na Jaji Mkuu Profesa Ibrahimu Juma kwenye ukumbi wa Mahakama ya rufaa jijini Dar es salaam.

Jaji Ibrahimu amesema Makamu wa Rais atafungua mkutano huo ambao unatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki wapatao 354 kutoka nchi mbalimbali za Jumuiya ya Madola.

Jaji Mkuu amesema katika mkutano huo Tanzania itawakilishwa na wajumbe 50 ambao ni Majaji na mawakili kutoka Tanzania bara na visiwani.

Ujumbe mwingine mzito wa watu 13 ambao ni Marais na Majaji kutoka Austaria, Zambia, Afrika Mashariki na Pakistani utakuwepo kwenye mkutano huo.

Aidha Jaji amebainisha kuwa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dkt. Mohamed Ali Shein atafunga mkutano huo mnamo Septemba 28 mwaka huu.