Jumanne , 28th Mar , 2017

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametinga kwenye mgodi wa dhahabu wa Buzwagi uliopo Kahama mkoani Shinyanga na kuchukua sampuli za mchanga kwa lengo la kwenda kuyapima kwa wataalamu wa madini ili kubaini kiasi cha dhahabu kilichomo.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiwa mgodini Buzwagi

Amesema wanataka kuona mchanga unaosafirishwa na mwekezaji huyo una kiasi gani cha dhahabu, pia Serikali inataka kufahamu kama kodi inayolipwa ni sahihi.

“Tumeamua kuchukua sampuli za mchanga ambao mwekezaji anasema wanaupeleka nje ya nchi kwa ajili ya kwenda kutenganisha madini ya dhahabu na shaba. Hata hivyo nimemuhoji kwa nini mitambo hiyo isiletwe nchini ili kila kitu kifanyike hapahapa,” Amesema Majaliwa

Waziri Mkuu amesema sera ya uwekezaji inasema mtambo huo unatakiwa uwepo nchini ili kila hatua ya uchenjuaji ifanyike hapa hapa, hivyo tunataka kujiridhisha na mwenendo wa mwekezaji na mapato tunayoyapata kama yanastahili.

Aliongeza kwamba “Hili lipo miongoni mwa masharti ya uwekezaji kwenye sekta ya madini nchini kwamba mitambo hiyo ije kujengwa hapa nchini na itaongeza fursa ya ajira na kukuza sekta nyingine ikiwemo ya kilimo,”.

Waziri Mkuu akiutazama mchanga wenye madini

 

Kuhusu uzalishaji mgodini hapo

Kwa upande wake Meneja Uendelezaji wa mgodi huo Bw. George Mkanza alisema mgodi huo ulionzishwa mwaka 2009 umeajiri watumishi 720 pamoja na vibarua 500.

Alisema kwa siku wanachenjua makontena matatu hadi sita ambapo katika kila kontena moja wanapata kilo tatu za madini ya dhahabu na tani nne za madini ya shaba.

Bw. Mkanza alisema wanazalisha asilimia 50 ya madini ya dhahabu na asilimia 50 ya dhahabu iko kwenye mchanga na inakuwa imechanganyika na madini ya shaba ambayo ndiyo unaosafirishwa kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kutenganishwa.

Malori makubwa, yakisomba mchanga uliochimbwa kwenye eneo la mgodi wa dhahabu wa Buzwagi.

“Hapa Buzwagi tuna makontena 179, makontena mengine 152 yako Dar es Salaam kwenye bandari kavu ya Nazam na 21 yako bandarini. Kila siku tunapoendelea kuzalisha tunakuwa na makontena manne hadi sita. Ndugu zetu wa Bulyanhulu nao wanamakontena 108 yako mgodini na 104 yako Nazam Cargo Dar es Salaam,” alisema.