Alhamisi , 8th Sep , 2016

Zaidi ya wafungwa 50 waliokuwa wamehukumiwa kwenda jela kwa kushindwa kulipia faini za kiwango tofauti tofauti wameachiwa huru baada ya kupata msaada wa kulipiwa faini zao.

Mchungaji Getrude Lwakatare

Msaada huo umetolewa na aliyekuwa Mbunge wa viti maalum CCM Dkt. Getrude Lwakatare kwa gharama ya shilingi Millioni 25 ambapo kwa awamu ya kwanza ametoa wafungwa 50 na awamu ya pili itawahusu wafungwa 28.

Akiongea na waandishi wa habari mara baada ya kutoa msaada huo katika magereza ya Ukonga, Keko na Segerea Dkt. Lwakatare amesema lengo kuu la kutoa msada huo ni kuisadia serikali kupunguza msongamano wa wafungwa magerezani.

“Hatutetei uhalifu, msaada huu siyo tu kupunguza wafungwa gerezani bali kurejesha nguvu kazi ya taifa na ndani ya familia kwani wazazi waliofungwa hapa ni masikitiko kwa familia na watoto wao, hivyo tumesaidia familia nyingi kurejesha amani na faraja kwao”

Aidha Dkt. Lwakatare amewaasa wale wote waliochiwa huru kutoka magerezani kuwa wananchi wema wanapoishi na kuacha kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani na kujikita katika ujenzi wa taifa.

“Biblia inasema katika Mathayo 25:36 – 40 inasema kuhusiana na kuwaona walioko kifungoni, na mimi kama mtumishi wa Mungu nimeguswa kutimiza andiko hilo” amesema

Lwakatare amewataka wanaoguswa na tukio hilo kujitokeza kwa wakati mwingine kuwasaidia wale waliofungwa kwa kukosa fedha za faini ili warudi tena uraiani na kushiriki katika shuguli za uzalishaji mali na maendeleo