Jumatano , 18th Oct , 2017

Jeshi la polisi Kanda maalum limemkamata meneja hoteli wa Peackock ya Dar es salaam, kwa kutoa ukumbi na kuruhusu watu wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja kufanyia mkutano, kitendo ambacho ni kinyume na sheria.

Kamanda Mambosasa ameyasema hayo leo alipokuwa akiongea na waandishi wa habari, na kusema kwamba serikali hairuhuhusu kuwepo kwa vitendo hivyo, na mtu yeyote atakayehusika kuhamasisha atachukuliwa hatua za kisheria.

Sambamba na meneja hoteli huyo ambaye hakutajwa jina lake, Kamanda Mambosasa amesema watu wengine 12 wamekamtwa kufuatia tukio hilo, wakiwemo raia wa kigeni wa Afrika Kusini

“Tumekamata wahalifu wengine pale Peacock ambao wanahamasisha ushoga hapa nchini, niendelee kutoa onyo kwamba kosa hilo kwetu ni kinyume na sheria, kwanza meneja wa hoteli tumemkamata kwa sababu alikuwa anajua ndio maana akatoa ukumbi, lakini pia wahusika warudi kwao wakaendelee huko kama sheria zao zinaruhusu, lakini kwa hapa nchini na kanda maalum ninasema ni marufuku na yeyote atakayepokea, kuhifadhi na kuwezesha kitendo hicho hatutamuacha”, amesema Kamanda Mambosasa.

Watu hao waliokamatwa ni pamoja na raia wawili wa Afrika Kusini, Mganda mmoja na Watanzania 9, na watafikishwa mbele ya sheria hivi karibuni.