Alhamisi , 21st Apr , 2016

Madereva wa daladala kugoma kwa zaidi ya saa nane kwa madai ya kunyanyaswa na watendaji wa SUMATRA

Wakazi wa mji wa Morogoro na maeneo ya jirani wamelazimika kutembea kwa miguu na wengine kupanda magari ya mizigo baada ya madereva wa daladala kugoma kwa zaidi ya saa nane wakishinikiza mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu (SUMATRA) kuacha kuwanyanyasa kwa kuwakamata na kuwatoza faini kubwa.

Wakizungumza katika maeneo mbalimbali ya mji wa Morogoro baadhi ya abiria wakiwemo wanafunzi wametupia lawama serikali kushindwa kushugulikia kero za madereva hao na kusubiri mgogoro unakuwa mkubwa na kuathiri shuguli za maendeleo na masomo kwa wanafunzi.

Wakieleza sababu za mgomo huo viongozi wa chama cha madereva wa daladala manispaa ya Morogoro wamesema mgomo huo umetokana na madereva kuchoshwa na utendaji mbovu wa afisa mfawidhi wa SUMATRA mkoa wa Morogoro kukamata hovyo daladala na kisha kuwatoza faini bila sababu za msingi.

Akizungumza mara baada ya kukutana na viongozi wa madereva hao mkuu wa wilaya ya Morogoro Muhingo Rweyemamu amesema kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya imewaomba warudishe magari barabarani hadi siku ya Jumatatu watakapokutana tena kutatua kero zao.

Abiria
Madereva
Mkuu wa wilaya pamoja na afisa wa SUMATRA