Jumatano , 23rd Mar , 2016

Mhasibu wa Baraza la Wafugaji Wilaya ya Ngoongoro, Loserian Raphael Laizer, amehukumiwa kwenda jela miaka 23,baada ya kutiwa hatiani kwa kusababishia hasara serikali zaidi ya shilingi milioni 4.3 kwa kuandaa orodha hewa ya majina ya wanafunzi.

Akizungumza jana Jijini hapa na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Arusha, Juventus Baitu, amesema Mhasibu huyo alihukumiwa Machi 18 mwaka huu, mbele ya hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Ngorongoro Dimitrio Nyakunga.

Amesema mtuhumiwa huyo alitiwa hatiani kwa makosa manne ya matumizi ya nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri, hivyo kila kosa alihukumiwa kifungo cha miaka minne na kosa la kuisababishia hasara serikali alihukumiwa kwenda jela miaka saba.

Baitu amesema mtuhumiwa alikuwa Mhasibu wa baraza hilo ambalo liko chini ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) na alifikishwa mahakamancha kwa mara ya kwanza na TAKUKURU Mkoa wa Arusha, kupitia wilaya ya Ngorongoro Juni 6 mwaka 2013.

Amesema shauri hilo lilifunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Ngorongoro na kusajiliwa kwa ECC.Na. 4 ya mwaka 2013 mbele ya hakimu Mfawidhi wa Wilaya Dimitrio Nyakunga.

Amefafanua kuwa jumla ya makosa aliyoshitakiw anayo ni matano, ambapo kati ya hayo manne yalihusiana na matumizi ya nyaraka zenye maelezo ya uongo kwa lengo la kumdanganya mwajiri kinyume na kifungu cha 22 cha sheria yakuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11 ya mwaka 2007.

Baitu amesema kosa la tano lilihusiana na kuisababishia hasara serikali kinyume na aya ya 10(i) kifungu cha 57 (1) na 62 (2) cha sheria ya Uhujumu uchumi kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
Amesema mtuhumiwa akiwa kazini alitayarisha nyaraka za uongo akiwa mhasibu wa baraza hilo kwa kuandaa orodha ya majina ya wanafunzi wanaodhaminiwa na Baraza la Wafugaji na kuwalipa ada na posho za kujikimu, wakati ni hewa.
Baitu amewaasa watumishi wa umma na wananchi kutojihusisha na vitendo vya rushwa na wananchi wakatae vitendo vya rushwa.