Jumatano , 13th Sep , 2017

Jeshi la Polisi jijini Dar es salaam limempiga risasi na kumuua muhusika wa matukio ya mauaji mbali mbali yaliyotokea mkoani Pwani yakiwemo mauaji ya watu Kibiti, pamoja na wizi katika baadhi ya benki hapa nchini.

Akitoa taarifa hiyo Kamanda wa Polisi Kanda maalum jijini Dar es salaam Lazaro Mambosasa, amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo katika eneo la Kivule Chanika, ambapo polisi ilimjeruhi Annae Rashidi Kapela maarufu kwa jina la Abuu Mariam alipokuwa akijaribu kukimbia, na kufariki dunia akiwa njiani wakimpeleka hospitali.

"Askari walipojaribu kumsimamisha aligeuka na kuanza kukimbia, askari walifyatua risasi na kumpiga kwenye goti, alipokamatwa jambazi huyo alitaja mlolongo wa matukio yaliyowahi kuyatekeleza, jambazi huyo amekiri kushiriki kwenye tukio la askari walioawa pale Mbande CRDB, uvamizi wa NMB Mkuranga, Access bank Mbagala, kule Kibiti ambapo askari 8 waliuawa na silaha  kuchukuliwa", amesema Kamanda Mambosasa

Kamanda Mambosasa aliendelea kusema kwamba baada ya jambazi huyo kukamatwa alihojiwa na kutaja baadhi ya wahalifu anaosaidiana nao kwenye uhalifu, na baada ya kumaliza kumuhoji alichukuliwa kuwahishwa muhimbili na kufariki dunia akiwa njiani.