Jumapili , 25th Oct , 2020

Mgombea wa Urais Zanzibar Dkt.Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa dhamira yake ya kuwatumikia Wazanzibari iko imara tofauti na wakati mwingine huku akieleza kuwa kampeni za Urais zimemuwezesha kujua uzito wa dhamana ya nafasi hiyo anayoiomba.

kushoto ni Mgombea mwenza wa urais Tanzania bara Samia Suluhu akisalimiana na Mgombea wa Urais Zanzibar Dkt.Hussein Ali Mwinyi.

Akizungumza na umati wa watu waliojitokeza katika mkutano wa kufunga kampeni zake katika uwanja wa Demokrasia (Kibandamaiti) Dkt.Mwinyi ametaja idadi ya mikutano ya hadhara na isiyo ya hadhara aliyoifanya kuwa ni 75 visiwani humo.

“Ninaposimama kuomba kura ninasimama nikiwa na uelewa wa uhakika wa haja zenu, matamanio yenu na matumaini yenu halikadhalika kampeni hizi zimeniwezesha kutambua uzito wa dhamana wajibu unaoambatana na dhamana ya Urais ninaouomba" amesema Dkt. Mwinyi

“Kuzunguka huku kumenipa fursa yakutafakari nakujipima tena na tena nimeridhika kuwa dhamira yangu yakuwatumikia wazanzibari iko imara sasa kuliko wakati mwingine wowote” ameongeza Dkt.Mwinyi

Leo Dkt.Mwinyi amefunga kampeni zake visiwani humo huku akisindikizwa na baadhi ya viongozi akiwemo Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt.Jakaya Kikwete, Samia Suluhu mgombea mwenza wa Urais Tanzania bara sambamba na Rais Dkt.Ali Shein anayemaliza muda wake Zanzibar.