Alhamisi , 15th Apr , 2021

Mbunge wa Jimbo la Mtama Nape Nnauye amesema Rais wa Awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Magufuli atakumbukwa kwa mafunzo aliyoyaacha Tanzania, Afrika na Dunia nzima.

Mbunge wa Mtama Nape Nnauye (kushoto) akiwa na aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dkt. Magufuli alimpomtembelea Ikulu, Dar es salaam.

Nape ameyasema hayo leo Aprili 15, 2021 bungeni, ambapo amesema 'legacy' ya Hayati Dkt. Magufuli inajitetea yenyewe kwa yale aliyoyafanya na yeye anajisikia fahari kwa kushiriki katika mchakato wa kumpata ndani na nje ya Chama Cha Mapinduzi kwenye uchaguzi mkuu mwaka 2015.

''Ninajisikia fahari kwamba nilishiriki ndani ya chama na nje ya chama katika mchakato wa kumpata Dkt John Pombe Magufuli mwaka 2015, amefanya kazi nzuri kwa taifa letu, ameacha alama nyingi kubwa ambazo hazitasahaulika,'' amesema Nape Nnauye.

Aidha ameongeza kuwa, ''Dkt. Magufuli ameacha mafunzo mengi, kwa nchi yetu, kwa chama chetu, kwa bara la Afrika na hata Dunia inajadili mafunzo aliyotuachia, namshukuru Mungu kwa maisha ya Dkt. Magufuli kwa nchi yetu.''

Amemaliza kwa kusema kuwa watu waendelee kufanya mazuri kwa nchi yao, kwani ukifanya hayo hauna haja ya kuyatetea bali yatajitetea yenyewe kwa vizazi na vizazi.

"Legacy haitetewi, legacy inajitetea yenyewe hasa ile iliyofanywa na mtu kama Dkt. Magufuli, legacy yake itajitetea, itajisimamia kwa miaka, unless mtu ana mashaka na legacy yake lakini kama hakuna mashaka legacy yake itasikiliziwa, itasemwa, itaongea na sisi watoto, wajukuu na vitukuu kwa sababu haya aliyoyafanya watayakuta tu hakuna haja ya kugombana," ameeleza.