Alhamisi , 14th Sep , 2017

Mbunge wa Iringa mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Mchungaji Peter Msigwa ameibuka na kumvaa Spika wa Bunge Mhe.Job Ndugai kwa kumwambia hana sifa ya kuwa kiongozi wa kusimamia nidhamu ndani ya bunge bali alipaswa kuwa gerezani muda huu.

Peter Msigwa ameleza hayo mchana wa leo alipokuwa mjini Nairobi nchini Kenya kumjulia hali Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu aliyeshambuliwa kwa kupigwa na risasi na watu wasiofahamika katika siku za hivi karibuni na kupelekea kuamsha hisia za watu wengi juu ya jambo hilo ambalo halikuwahi kutegemewa kutokea Tanzania nchi yenye amani na usalama wa kutosha. 

"Ninaomba mumuogope Mungu kwa sababu tunaleta mchezo na maisha ya Watanzania, mnataka kutunyamazisha ili tusiseme. Tutasema mpaka mwisho wetu kwa sababu uhai wetu na usalama wa taifa letu umetishiwiwa kwa kiwango cha juu sana lakini Mhe. Ndugai wewe kama spika unasifa gani ya kutuambia sisi tuwe na adabu ndani ya bunge wakati wewe mwenyewe kipindi cha kampeni ulionekanaa ukipiga watu hadharani na fimbo, ulitakiwa uwe gerezani na siyo kutusimamia nidhamu ndani ya bunge", amesema Msingwa.

Pamoja na hayo, Msigwa ameendelea kwa kusema "Nakuchukulia Mhe. Job Ndugai kama wewe ni adui, yaani wewe ni adui wa usalama wa taifa la Tanzania kwa sababu unasababisha muhimili wa bunge uwe dhaifu kutokana na serikali ya Tanzania imekuteka na kukupa maagizo na kulifanya bunge liwe butu, lishindwe kusimamia maamuzi na kulisimamia serikali. Nasema haya kwa ujasiri mkubwa sina kitu cha kuogopa tena kama ndugu yetu ameshapigwa risasi na tumeshaambiwa tunaofutwa ni sisi hivyo hatuna cha kuogopa kusema jambo lolote", amesisitiza Msigwa.

Kwa upande mwingine, Mchungaji Msigwa amedai muda mwingine wanashindwa hata kuwaambia watoto wao kuwa Mhe. Job Ndugai ni kiongozi wao wa bunge kwa kuwa wanatishwa, wanafukuzwa pamoja na kupigwa pingu huku akisisitiza kuwa yupo tayari kufukuzwa bungeni lakini hatoweza kukaa kimya.