Jumapili , 19th Mar , 2017

Mbunge wa Singida Magharibi Elibariki Kingu ameibuka na kuweka wazi kuwa yuko tayari kufukuzwa ndani ya chama chake cha CCM kwa kupinga uhalali wa elimu ya Mkuu wa Mkoa wa dar es Salaam.

Katika taarifa yake aliyoitoa leo, Kingu amesema anasikitishwa na ukimya uliotanda miongo mwa wanachama wa CCM kwa hofu ya kufukuzwa uanachama na kuacha Rais Magufuli akisemwa vibaya kila kona ya nchi kwa sababu ya kiongozi mmoja ambaye elimu uhalali wa elimu yake unatiliwa shaka.

"Najua hofu mliyonayo watanzania juu ya huyu RC. Ikiwa mamlaka zitaendelea kufumbia macho. Mimi Elibariki Immanuel Kingu mbunge wa CCM nitakuwa wa kwanza kufukuzwa CCM kama kupinga matendo maovu ya RC huyu itaonekana ni usaliti kwa nchi. Haiwezekani Rais wetu atukanwe kila kona kwa matendo ya mtu huyu. Wana CCM ukimya wetu kwenye hili halikubaliki". Amesema Kingu.

Kingu ambaye amezungumza na EATV kwa njia ya simu na kuthibitisha taarifa, ameongeza kuwa anakerwa na kusikitishwa na kelele zinazoendelea mitandaoni kuhusu tuhuma za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kughushi vyeti vyake vya taaluma huku matusi na kejeli zikipelekwa kwa Rais, na bado wana CCM wako kimya.

Pia ameonesha kukerwa na kile alichokiita matendo yanayokiuka utawala wa sheria yanayofanywa na mkuu huyo wa mkoa.

"Naomba sasa niweke kumbukumbu sawa najua mnamchafua kila anayempinga RC huyu kwa matendo yake ambayo yanakiuka utawala bora. Naomba niwe wa kwanza kufukuzwa CCM kwa kumpinga RC Makonda"