Jumapili , 26th Feb , 2017

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, amemteua Bw. Omary Rashid Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL).

Omary Nundu

Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi imeeleza kuwa uteuzi wa Bw. Omary Rashid Nundu umeanza tarehe 24 Februari, 2017.

Bw. Omary Rashid Nundu anachukua nafasi ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL Prof. Tolly Salvatory Augustine Mbwete.

Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amemuapisha Thobias Emir Andengenye kuwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Thobias Andengenye kuwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, tukio lililofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam Februari 26,2017

Kamishna Jenerali Thobias Emir Andengenye anachukua nafasi ya Kamishna Jenerali Pius M. Nyambacha ambaye amestaafu.

Pia, Mhe. Rais Magufuli amewaapisha Mabalozi wanne walioteuliwa kuiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali kama ifuatavyo;

Mhe. Dkt. Pindi Hazara Chana ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Nairobi, Kenya ambako anachukua nafasi ya Mhe. John Haule ambaye amestaafu.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Pindi Chana kuwa Balozi wa Tanzania nchini Kenya, tukio lililofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam.

Mhe. Silima Kombo Haji ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Khartoum, Sudan ambako anakwenda kufungua Ubalozi.

Mhe. Abdallah Abas Kilima ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Muscat, Oman ambako anachukua nafasi ya Mhe. Ali Ahamed Saleh ambaye amestaafu.

Mhe. Matilda Swila Masuka ameapishwa kuwa Balozi wa Tanzania Seoul, Korea Kusini ambako anakwenda kufungua Ubalozi mpya

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimuapisha Balozi Matilda Masuka kuwa Balozi wa Tanzania nchini Korea Kusini, Ikulu jijini Dar es Salaam.

Aidha Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Mabalozi wote wanne wakila kiapo cha uadilifu kwa viongozi wa ummakilichoongozwa na Kamishna wa Maadili Mhe. Jaji Mstaafu Harold Nsekela.

Hafla ya kuapishwa kwa viongozi hao imehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Mwigulu Lameck Nchemba na viongozi wa vyombo vya ulinzi na usalama.

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Thobias Andengenye akila kiapo cha Ahadi ya Uadilifu pamoja na Mabalozi Pindi Chana, Balozi Silima Kombo Haji, Abdallah Kilima pamoja na Balozi Matilda Masuka mara baada ya kuapishwa Ikulu jijini Dar es Salaam.

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika picha na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kasim Majaliwa, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Mhandisi John Kijazi (wapili kutoka kushoto), Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi Mwigulu Nchemba(Wakwanza kulia) , Naibu Waziri wa Mambo ya ndani Hamad Masauni (Wakwanza kushoto) pamoja na Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Thobias Andengenye(Watatu kutoka kushoto waliosimama mstari wa nyuma) na Mabalozi Pindi Chana(Wakwanza kulia walisimama mstari wa nyuma ) , Balozi Matilda Masuka(Wapili kutoka kulia waliosimama mstari wa nyuma), Balozi Abdallah Kilima(Wapili kutoka kushoto mstari wa nyuma) na Balozi Silima Kombo Haji (Wakwanza kushoto waliosimama) mara baada ya tukio la Uapisho Ikulu jijini Dar es Salaam.