Jumatatu , 12th Apr , 2021

Waziri wa Maji Juma Aweso amekiri moja ya changamoto ya miradi ya maji ni usimamizi huku akisema uanzishwaji wa Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) umesaidia katika kutatua baadhi ya changamoto.

Waziri wa Maji Juma Aweso

Aweso ameeleza hayo akijibu swali lililoulizwa na Mbunge wa Viti Maalum Ester Bulaya ambaye alitaka kujua kama Serikali ipo tayari kufanya ukaguzi maalum nini chanzo cha miradi kukamilika na maji hayatoki au ni nini kinachosababisha miradi ichukue muda mrefu kwani Wizara ya Maji imekuwa ikitengewa pesa nyingi tangu 2016 lakini ufaniisi na ubora na kinachokusidiwa hakipo.

"Nikiri moja ya changamoto kubwa ya miradi ya maji ni usimamaizi, lakini Mhe. Spika bunge lako tukufu limeona hili ndiomaana tukaanzisha wakala wa maji vijijni RUWASA na kuhakikisha Wahandisi waliokuwa chini ya Halmashauri wanakuwa chini ya Wizara, nataka nimuhakikishie mbunge tumeshaainisha miradi zaidi ya 177 na RUWASA imeshaanza kuitatua miradi hiyo zaidi 85," amesema Aweso.

Pia, Waziri Aweso alitumia nafasi hiyo kutoa onyo kwa wahandisi wa maji pamoja na wakandarasi wa maji kutokuchezea miradi ya maji kwani watashughulikiwa ipasavyo.