Ijumaa , 9th Apr , 2021

Ugonjwa wa ajabu umeua watu wanane kwenye kijiji kidogo kilichoko katika  Kaunti ya Kakamega nchini Kenya.

wakazi wa kijiji cha Shina

Mamlaka husika zilithibitisha vifo katika wadi ya Isukha Magharibi, lakini sababu ya ugonjwa huo bado haijafahamika.

Moja ya dalili ambazo wagonjwa wameeleza kuwa nazo ni pamoja na kutokewa na vipele vinavyowasha ambavyo hupelekea malengelenge na kuvimba kwa mikono, na kusababisha kifo hapo baadae.

Aidha, mmoja wanakijiji alisema hofu ilishika kijiji cha Shina kutokana na  uvumi ulioenea kwamba ugonjwa huo kuhusishwa na imani za kichawi baada ya pombe ya kienyeji kuibwa kutoka nyumbani na mmiliki wa nyumba kutishia kwenda kwa mganga.

Nao wagonwa amabao wanasumbuliwa na ugonjwa huo wamelalamikia maumivu makali wanayoyapata ilihali tiba za asili zikishindwa kusaidia na wengine wakishindwa kwenda hospitali kwa hofu.

“Mume wangu alianza kufanya vitu sio vya kawaida, aliniambia hakuwa mzima na aliogopa angekufa na hata alitishia kujiua kwa sababu ya maumivu,” alisema mjane Violet Wiraka ambaye alishuhudia mumewe akiugua ugonjwa hadi kukumbwa na umauti. 

Kwa upande wake Gavana wa Kaunti ya Kakamega Wycliffe Oparanya amesema wanasubiri ripoti kutoka kwa timu ya wataalum wa afya walioituma ili waweze kukabiliana na hali hiyo kwani bado nchi ipo kwenye wimbi la virusi la corona.