Jumapili , 29th Jan , 2023

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mary Chatanda amewataka viongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania kusimamia vizuri fedha za miradi ya maendeleo zilizotolewa kwenye mikoa mbalimbali na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan

Ameyasema hayo wakati wa Maadhimisho ya Miaka 46 ya Chama cha Mapinduzi yaliyofanyika katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Amesema wabunge, madiwani na watendaji wengine kuanzia ngazi ya kata wanatakiwa kushirikiana na viongozi wa Serikali kuhakikisha fedha za miradi ya maendeleo zinatekeleza miradi hiyo ipasavyo.

Aidha, amewataka wanawake kuhakikisha wanaelimisha wananchi juu ya miradi mbalimbali ya maendeleo iliyotekelezwa na Mheshimiwa Rais katika maeneo yote nchini ili wawe na uelewa juu ya miradi hiyo.

Naye, Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Zainab Shomari amewataka wanawake kuchangamkia fursa mbalimbali zinazojitokeza ili kujiinua kiuchumi.

Ameongeza kuwa ni vema wanawake wakafanya kazi kwa kupendana na kushirikiana kuhakikisha jumuiya ya UWT inakuwa imara.