Alhamisi , 14th Sep , 2017

Mbunge wa jimbo la Chemba, Juma Nkamia (CCM) amethibitisha kuwa leo atapeleka hoja binafsi kwa spika wa bunge kuhusu uchaguzi mkuu nchini ufanyike kila baada ya miaka saba na isiwe mitano kama sasa ili kuepuka gharama kubwa ambazo huwa zinatumika.

Mbunge Juma Nkamia

Akifanya mahojiano kwa njia ya simu na mtangazaji wa EATV, Mh. Nkamia amesema kuwa yeye ameamua kupeleka muswada huo binafsi kwa spika wa bunge kutokana na serikali kutumia gharama kubwa za kufanya uchaguzi kwa wakati mmoja yaani ule wa serikali za mitaa pamoja na ule mkuu.

"Napeleka hoja au muswada binafsi kwa Spika wa bunge tulijadili hili kama linaweza kufanywa sheria lifanyike.  Ndani ya bunge kuna viongozi wetu wa chama kwa hiyo lazima nipeleke kwao ili kujadili na wao waweze kupitisha kama watakubaliana na mimi na kama ikifanikiwa kufika kwa rais basi iwe sheria ambayo itatuoongoza," amesema Nkamia.

"Nikipeleka hoja yangu kwa Spika nitachanganua gharama zinazotumika kufanya uchaguzi wa serikali za mitaa pamoja uchaguzi mkuu. Tunaweza kufanya uchaguzi wote kwa pamoja kama wenzetu mfano Kenya wanakuwa na maboksi mengi sana wakati wa kura, hata sisi tunaweza kufanya kama wenzetu badala ya kutumia gharama mbili kwa kipindi kimoja" aliongeza Nkamia.

Aidha, Mh. Nkamia amefafanua kuwa aeleweke kuwa hajamlenga rais aliyoko madarakani ndiye aanze kwenda miaka saba bali ni kwa viongozi wote na kama wazo lake likitimia wakati Rais Magufuli akiwa madarakani nayo si vibaya.

"Muswada una 'process' zake kwani lazima upitie sehemu nyingi na kama ukishafika kwa wabunge ukajadiliwa na ikakubalika sheria ifanyiwe mabadiliko ndani ya sheria na rais akatia saini ndiyo itakuwa sheria kamili. Na ukifanikiwa kupita wakati Rais Magufuli akiwa madarakani ni vema tu kwani kuna matatizo gani?:", amehoji Nkamia.

Pamoja na hayo Mh. Nkamia amesema kuwa watu wengi na waoga wa kutoa hoja zao kwa kufikiria wananchi watamfikiriaje hivyo kwa upande wake huwa hana woga wowote linapokuja suala la kusimamia hoja.