Alhamisi , 23rd Mar , 2017

Chama cha madaktari nchini Kenya kimewataka madktari kutoka Tanzania kusubiri baada ya miezi miwili ndipo waende nchini humo kwa ajili ya kufanya kazi ambayo imetangazwa kwa madaktari wa Tanzania kama fursa.

Hayo yamethibitishwa na Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), Dkt. Obadia Nyongole katika kipindi cha Hot Mix cha EATV na kusema kuwa taarifa hiyo imetoka kutoka chama cha madktari cha Kenya na kuwataka watanzania kusubiri kwanza watimiziwe malipo yao na serikali ya nchi hiyo

Dkt. Obadia ameendelea kusema kwamba pamoja na chama hicho cha madaktari cha Kenya kufurahi kuona watanzania wamejitolea kwenda kuwasaidia katika mgogoro unaoendelea bado kinaona kuwa ni sawa na kwenda kuwazibia wazawa fursa za kazi kitu ambacho kitaweza kusababisha vita vya kitaaluma.

Katika hatua nyingine Obadia ameongeza kwamba pamoja na kuwa si jambo la kushangaza serikali kusaidia wasomi wake kupata ajira nchi tofauti tofauti, fursa ya madaktari 500 kwenda Kenya kwa upande wao bado wana hofu nayo.

“Fursa hii haijaja wakati muafaka, imekuja mapema mno kwani mgogoro bado upo unaendelea nchini Kenya. Vitisho ni vingi wanaamini na bado madaktari hao hawana imani kama serikali yao itaweza kutekeleza ahadi, tunawasiliana na madaktari wenzetu dunia nzima, hata kenya tunawasiliana nao, chama cha madaktari Kenya hawana shida lakini pia wasiwasi wao ni  mwezi Mei kutakuwa na zaidi ya wanafunzi 1400 wanao hitimu watakuwa hawana ajira” Obadia alisema.

Tazama mahojiano haya..............