Jumatatu , 19th Jun , 2017

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema kuna zaidi ya nchi 80 ambazo watanzania wanaweza kusafiri bila ya kuwa na viza .

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni amesema kuna zaidi ya nchi 80 ambazo watanzania wanaweza kusafiri bila ya kuwa na viza za kusafiria kama ilivyokuwa nchi za afrika Mashariki.

Mhandisi Massauni amebainisha hayo leo bungeni wakati akijibu swali la Mbunge wa Mlalo kupitia tiketi ya CCM Rashid Shangazi aliyetaka kujua ni nchi ngapi ambazo watanzania wanaweza kusafiri bila ya kuwa na viza (viza on arrival).

"Zipo nchi 16 kwa Afrika ambazo watanzania wanaweza kuzitembelea bila ya kuwa na viza na duniani zipo 67" alisema Masauni.

Aidha Massauni amezitaja nchi hizo kuwa ni Benin, Burkina Faso, Cape Verde, Ivory Coast, Djibouti, Gabon, Gambia, Guinea, Guinea­Bissau, Liberia, Mali, Mauritania, Niger, Sierra Leone pamoja na Togo.

Pamoja na hayo Masauni amesema zipo nyingine ndani ya umoja wa Jumuiya ya Madola lakini haziwezi kuwapatia fursa watanzania kutumia 'viza on arrival'.

"Ni kweli nchi za Jumuiya Madola zinautaratibu wa kutembeleana wananchi wake bila ya kuwa na Viza lakini kama nilivyo jibu katika swali langu la msingi kwamba ushirikiano na matengemano hayo ya jumuiya ya madola utaratibu wake unaweza kubadilika kulingana na mahusiano na hali ya kiusalama kwa hiyo siyo jambo la kushangaza kuona  India na Nigeria kwamba nchi hizi  mbili zipo kwenye uanachama wa Jumuiya ya Madola lakini utaratibu wa viza kuna 'level' unakuwa hautumiki" alisisitiza Masauni.