Ijumaa , 20th Jan , 2017

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametoa agizo kwa viongozi wote nchini ngazi ya mikoa na wilaya kuacha mara moja kuwakamata wauguzi na wakunga na kuwaweka ndani na badala yake wanapaswa kufuata taratibu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu

 

Akizungumza hayo wakati wa uzinduzi wa mradi wa 'Mkunga Okoa Maisha', Waziri Ummy Mwalimu amesema wakunga wanalo baraza la wauguzi na wakunga ambalo ndilo lenye dhamana ya kushughulikia nidhamu na maadili ya kazi za wauguzi na wakunga nchini.

Amesema wauguzi wengi ni wazuri na wanajituma lakini ni kweli kuwa wapo wachache wenye matatizo ambao ni lazima washughulikiwe kwa mujibu wa taratibu zilizopo na kuongeza kuwa pale ambapo muuguzi au mkunga anapokosea zipo taratibu za kufuata na siyo kumweka

"Tunao wakunga na wauguzi ambao wanafanya kazi zaidi ya masaa, tumeona kilichotokea Sikonge, kiongozi anakuja juu kwanini mtoto amepewa dawa ya Quinn. Tuache kuingilia kazi za kitaalamu" amesema Ummy.

Mhe Ummy amesema kuwa kwa kuwa takribani asilimia 80 ya kazi ya kumuhudumia mgonjwa katika vituo inafanywa na wauguzi na wakunga, Serikali itaendelea kuwajengea uwezo na pia kuboresha mazingira yao ya kazi ili kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Baraza la Wakunga nchini Dkt. Sebalda Leshabari amesema kuwa mradi huo unaofadhiliwa na Serikali ya Canada unalenga kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi katika mikoa ya Shinyanga na Simiyu hivyo wauguzi na wakunga ni vema wakashirikiana na baraza hilo ili kufanikisha malengo yao.