Alhamisi , 21st Sep , 2017

Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam imesitisha mkataba na Kampuni ya Mwamkinga Auction Mart and Brokers ambayo ilikuwa inashughulika na kudhibiti maegesho ya magari katika maeneo yasiyosahihi Kanda ya Temeke.

Akiongea leo na waandishi wa habari ofisini kwake Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam,  Isaya Mwita amesema Mkandarasi huyo amevunja masharti ya mkataba kutokana na kufanya kazi zake bila kuzingatia weledi.

“Wakandarasi wetu lazima waheshimu hawa Watanzania wanaotumia magari sio “ATM” nimesikia kelele nyingi sana kuhusu Mwamkinga jinsi anavyokamata malori kule, kimsingi anawaotea na kuwapiga faini kubwa pengine laki tatu hadi nne na watu wanakuwa wameegesha kwa dharura chini ya dakika 30 anawapiga faini”, amesema Mwita.

Mstahiki Meya ameongeza kuwa Halmashauri ya Jiji la Dar es salaam imeamua kusitisha mkataba huo kuanzia Septemba 19 kwasababu ameshapewa onyo lakini hawajaonesha nia ya kubadilika. Aidha Mwita amewataka Wakandarasi wengine waendelee kufanya kazi kwa weledi vinginevyo atavunja mikataba yao pia.

Amesema haiwezekani kwamba mtu amesimama kwa dakika moja alafu gari lake linafungwa kwa mnyororo na kumwandikia faini ya Sh 200,000 hadi Sh 300,000 ambayo haipelekwi halmashauri. 

“Hiyo kampuni ilikuwa inafanya kazi hadi saa tatu usiku tofauti na makubaliano ya mkataba unavyosema mwisho saa 12 jioni . Nitaendelea kufuatilia kwa wilaya za Kinondoni na Ilala ambapo kama wataenda tofauti na mikataba inavyosema watasitishiwa mikataba yao"  ameongeza.

Mwita amesema lengo la halmashauri  siyo kumkandamiza mwananchi bali kusimamia sheria ili watu wazifuate lakini imeonekana tofauti ambapo amekiri kusikia watu hao wanakusanya hadi shilingi milioni nne kwa mwezi ambazo haziwasilishwi katika halmashauri ya jiji.