Jumatatu , 20th Nov , 2017

Serikali imesema itaendesha msako na kuvifunga vyuo vyote vya afya visivyokidhi vigezo na msharti ya uwepo wake.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile, alipozungumza kwenye mahafali ya Chuo cha Tiba na Afya cha KAM.

Amesema ingawa ni kweli kuna uhaba mkubwa wa watumishi wa sekta ya afya, lakini serikali haiwezi kuvumilia vyuo ambavyo vinajiendesha bila kufuata miongozo ya serikali.

“Ni kweli tuna uhaba wa watumishi zaidi ya 95,000 wa sekta ya afya lakini hakiwezi kuwa kigezo cha watu kujiendesha kwa ubabaishaji ubabaishaji, lazima miongozo ifuatwe,” Mh. Ndugulile.

Aidha, waziri huyo alisema serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na vyuo binafsi hivyo itaendelea kushirikiana navyo kutatua changamoto mbalimbali ili viweze kustawi na kutoa wahitimu wengi zaidi watakaosaidia taifa.