Jumatano , 26th Jul , 2017

Watu watatu wa familia moja wamejeruhiwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni tindikali kwa kumwagiwa usoni, kifuani na mikononi mwao tukio lililotokea usiku 3:30 ya tarehe 19.07.2017, eneo la Manga, Mkoani Mbeya.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya DCP Mohammed Mpinga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya DCP Mohammed Mpinga amewataja watu hao kuwa ni Vumilia Shangema (31) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Manga akiwa amefuatana na watoto wake wawili Loveness John (11) mwanafunzi wa darasa la sita katika shule ya Msinge Sinde na Nancy Peter (5) ambapo inadaiwa tukio hilo liliwapata wakiwa wanatokea dukani kununua bidhaa kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.

Inasemakana wakati wakiwa njiani waliweza kukutana mama mmoja aliyefahamika kwa jina la Emmy Kyando (40) mkazi wa Sae mkoani humo ambaye inadaiwa kuwa ni mke mwenza wa muhanga wa tukio hilo na mara baada ya kuonana naye walimwagia kimiminika hicho katika sehemu za mbalimbali katika miili yao na baada ya hapo waliweza kupata msaada toka kwa wasamaria wema wa kupelekwa Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa matibabu.

Kamanda Mpinga amesema chanzo cha tukio hilo inadaiwa kuwa ni wivu wa kimapenzi dhidi yao, huku akisisitiza kuwa juhudi za kumtafuta mtuhumiwa zinaendelea kwa kushirikiana na mume wake aliyefahamika kwa jina la Lausi Kidagile.