Jumanne , 12th Sep , 2017

Msanii wa muziki wa kizazi kipya ambaye leo ameachia kazi yake mpya ya 'I miss you', ametoa maoni yake juu ya hali ya sasa inayoendelea hapa nchini, ikiwemo matukio ya kupigwa na risasi kwa Tundu Lissu na Meja Jenerali Mstaafu Vicent Mritaba.

Lady Jaydee

Akizungumza kwenye kipindi cha Planet Bongo kinachorushwa na East Africa Radio, Lady Jaydee amesema hali ya nchi ilivyo sasa ni ya kutisha na inaashiria kutoweka usalama tunakoelekea, huku akikumbushia na tukio la kutekwa kwa msanii mwenzake Roma Mkatoliki.

"Kitendo cha mtu kuweza kupigwa risasi hadharani inatishia amani, vile vile kuna wasanii wengine walikuwa wametekwa, unaogopa, sehemu yenye amani vitu kama hivyo haviwezi kutokea, naweza nisiwe na maneno ya kusema lakini nikaishia kusikitika tu, kwa sababu sio mambo mazuri haya yanayotokea, na yanaonyesha dhahiri tunakoelekea sio kuzuri", amesema Lady Jaydee.

Hivi karibuni kumekuwa na matukio ya kutishia usalama wa nchi ikiwemo kuuawa kwa watu mkoani Pwani, kupigwa risasi kwa Tundu Lissu, kutekwa kwa watu wakiwemo watoto na msanii Roma, na kupigwa risasi kwa Meja Jenerali Mstaafu Vicent Mritaba.