Alhamisi , 14th Sep , 2017

Msanii wa filamu bongo, Daudi Michael maarufu kama 'Duma' amefunguka na kudai hana ugomvi wa aina yeyote na muigizaji mwenzake, Gabo Zigamba ila alichokifanya ni kumtaka abadilike ili aweze kutoa kazi zake wananchi wapate kukiona anachokifanya.

Duma amebainisha hayo baada ya kutoa kauli yake siku za hivi karibuni ya kudai Gabo ndiye chanzo cha tasnia ya filamu kulega lega kwani ameaminiwa na watanzania wengi lakini ameshindwa kuwatendea haki kwa kutoa kazi tangu alipopata tuzo ya muigizaji bora wa kiume pamoja na filamu bora ya mwaka zilizoandaliwa na kutolewa na uongozi wa EATV LTD mnamo mwezi wa 12 mwaka 2016.

"Sina cha kumuonea wivu Gabo, ila mimi siwezi kumuongelea Ray Kigosi, Jacob Stephen (JB) au Rado kwa sababu hao ni watu wa kubwa kwangu lakini 'career' yangu inapokuwa inakosea ni lazima niseme ili mradi mambo yawe sawa tusiweze kukwama huko tunapoenda, mimi nina uchungu sana na hii 'industrial' nafanya kwa sababu ya watanzania wote hata niliyoyaongea sina ugomvi na Gabo na wala siyo mbaya wake", amesema Duma.

Pamoja na hayo, Duma ameendelea kwa kusema "Gabo anatakiwa ajiongeze ili aweze kutanua wigo mkubwa hata nje ya Tanzania aweze kufahamika juu ya anachokifanya. Tunahitaji watu wa kuitoa 'industrial' hapa ilipo na kuipeleka nje ya nchi kama yeye anaona hawezi atatuachie kazi yetu arudi nyumbani", amesisitiza Duma.

Kwa upande mwingine, Gabo amesema imetosha kwa yeye kumzungumzia Gabo kwa sasa kwa madai hana jambo jipya la ku-postiwa katika mitandao ya kijamii lakini kupitia yeye anaweza akapata bahati hiyo kwa sababu hana kazi yeyote aliyoifanya katika tasnia ya filamu.