Jumatatu , 21st Aug , 2017

Rapa Godzilla ambaye kwa sasa anasumbua na ngoma ya  'X ' amekanusha kuchanganyikiwa kutokana na kuachana na mpenzi wake na kudai kuwa yeye siyo wa kwanza kushindwa kufika mbali na mpenzi wake na kwamba maneno yanaletwa na umaarufu wake.

Rapa Godzilla

Akizungumza na mwandishi wetu Godzilla amesema kwamba watu walikuwa wanamuona kama kachanganyikiwa kutokana na kutokujua ni nini kilichokuwa kinaendelea kwenye maisha yake hivyo wengi walikuwa wakimchokonoa ili kuweza kumfahamu zaidi kutokana tu tayari yeye ni msanii lakini pia siyo mtu wa kuonyesha maisha yake binafsi hadharani.

"Nashangaa hata hayo maneno yalipokuwa yanatoka, lakini kwa vile mimi ni maarufu lazima mishale inayorushwa kwangu mingine inipate hivyo kwa kuwa hilo nimeshalifahamu ndiyo maana nimekuwa kimya kwa sababu sipendi maisha yangu kuwa wazi kwa kila mtu. Unajua kuna mtu anaishi Temeke lakini ukimkuta anasimulia maisha yangu ya Salasala utadhani ananijua sana lakini siwezi kuwajibu tayari mimi ni msanii hivyo napokea mishale yao" Zilla

"Ni kweli nilikuwa kimya watu wakaanza kuni attack pasipokujua mimi nafanya nini. Nilikuwa nashughulika na studio yangu kukamilika na tayari tumeshamaliza hilo. Kila kinachohitajika ndani ya studio tumeshanunua na kazi zitaanza kusikika na vitu vingi ambavyo tutakuwa tunatengeneza hapo vitaanza kusikika na kuonekana hivi karibuni".

Akizungumzia kuhusu wimbo wa 'X'  Zillah amesema kuwa hakumlenga mtu yeyote kwenye wimbo huo na badala yake ni kama kutoa ujumbe kwa mtu anayetaka mafanikio lazima kufuta baadhi ya watu wanaomfanya mtu asifanikiwe.

"Sijamlenga aliyekuwa mpenzi wangu kwenye wimbo huu. Mimi ni msanii natakiwa kuburudisha watu. Kwenye wimbo huu maisha yangu sijayaweka lakini ni ujumbe ambao nimeufikisha mtaani kuwasaidia watu wanaohitaji kufanikiwa katika maisha na ndiyo maana ya 'X',  Siyo lazima ung'ang'ane na watu ambao hawakufanyi wewe upate mafanikio" Zilla aliongeza

Zilla ameahidi kuachia kichupa cha wimbo huu haraka baada ya kuitambulisha 'Audio' mapema wiki iliyopita.