Jumanne , 19th Sep , 2017

Msanii wa miondoko ya singeli Man Fongo amefunguka na kudai hakuna mtu yeyote ambaye anaweza kumhofia katika kazi zake kwa kuwa wote hawajaweza kufikia kile anachokifanya yeye mpaka sasa.

Man Fongo amebainisha hayo kupitia kipindi cha eNewz kutoka EATV baada ya kuwepo maneno ya muda mrefu kwa wasanii wanaoimba singeli kila mmoja wao kujipa jina la mfalme katika uwimbaji wa muziki huo.

"Hakuna msanii yeyote anayeimba singeli kwamba nikimuona moyo wangu unaweza ukaingia na kitete au hofu, kwa sababu hakuna mwenye wasifu mkubwa kama mimi 'CV', wanatakiwa walitambue hilo. Na kama wanataka niwaogope basi kwanza wafanye vitu vikubwa zaidi yangu, ndiyo nitaweza kuwaogopa lakini kama huna 'CV' kama zangu bado utabakia kuwa 'kinda", amesema Man Fongo.

Kwa upande mwingine, Man Fongo amewataka wasanii wenzake wawe wabunifu katika kufanya muziki wao ili mradi singeli iweze kuonekana siyo muziki wa kurudia rudia maneno kila mara.

Mtazame hapa chini msanii Man Fongo akiendelea kufunguka kuhusu suala lake.