Jumanne , 17th Jan , 2017

Msanii wa muziki wa bongo fleva Lady Jaydee amefunguka na kusema wanawake wengi wanaogopa kuanza maisha mapya ya mahusiano kwani wengi wao wanashindwa kuondoka kwenye ndoa zao ambazo hazina afya.

Msanii Lady Jaydee akiwa na mpenzi wake Spicy

Lady Jaydee alisema hayo kupitia kipindi cha Wanawake Live kinachorushwa na EATV na kusema wanawake wengi wanashindwa kufanya maamuzi kwa sababu hawajiamini na wanaogopa kwenda kuanza maisha mapya.

"Wanawake wengi wanashindwa kutoka kwenye mahusiano kwenye ndoa zisizo na afya ni kutokana na wao kutojiamini, kwanza si jambo rahisi sana kama umekaa na mtu muda mrefu harafu uamue tu kuwa unaondoka, ni kwamba kuna maisha ambayo mmejenga pamoja kwa hiyo unapoondoka unakwenda kuanza maisha mapya, watu wengi lile suala la kwenda kuanza maisha mapya ndiyo huwa wanaliogopa" alisema Lady Jaydee.

Mbali na hilo Lady Jaydee anadai licha ya watu wengi kuogopa kuanza maisha mapya lakini yeye aliamua kufanya maamuzi ya kusonga mbele kwani hakuhitaji kubaki kwenye mahusiano ambayo kwake yalikuwa hayana faida yoyote.