Jumatano , 29th Mar , 2017

Muigizaji maarufu wa filamu Bongo, Jacob Stephen  Bonge la bwana maarufu kama  JB amefunguka na kuweka wazi kwamba maisha yake ya kutopata mtoto mpaka sasa kwenye ndoa yake hayajawahi kumkosesha furaha wala kuacha kumpenda mke wake.

JB

Kwenye kipindi cha Kikaangoni kupitia Facebook ya EATV wakati akijibu maswali ya mashabiki wake JB amesema kuwa hajabahatika kupata mtoto kwenye ndoa yake lakini bado hajakata tamaa na anaamini ipo siku Mungu atajibu maombi yake.

"Sina mtoto, sijabahatika kupata mtoto kwenye ndoa yangu, lakini kutokuwa na watoto kwenye maisha yangu haijawahi kunifanya nikose amani au nimchukie mke wangu. Nampenda sana lakini ipo siku naamini Mungu atatupatia au tusipopata kabisa sitaweza kukufuru kabisa" - JB.

Aidha JB ambaye amekiri kukaribia kufikisha umri wa miaka 50 amewataka watu wote ambao hawajajaliwa kupata watoto wasiache kumshukuru Mungu na siku zote waishi maisha ya furaha.

JB akiwa Kikaangoni

"Wakati mwingine nawaza kuna watu wamejaaliwa watoto lakini hawana furaha sisi tuliyonayo, niwaombe hata wale ambao bado hawajabahatika kupata watoto wasiishi kwa kukosa amani wafurahie maisha Mungu aliyowapatia watoto ni baraka itokayo kwa Mungu" - JB aliongeza.

Aidha Muigizaji huyo amesema hawezi kumsaliti mke wake kwa kuwa na wanawake wengine kwa sababu kufanya hivyo ni kujiunganisha kiroho na watu tofauti tofauti kupitia mapenzi.

Kuhusu kuokoka, JB amesema ameokoka na anampenda Yesu, na kwamba tangu aoe hajawahi kuchepuka na hadi sasa ana mke mmoja bila hawara. "Kadri unavyotembea na wanawake wengi unatengeneza sura nyingi na za ajabu, pia unachukua bahati na mabalaa ya hao watu"

Katika hatua nyingine msanii huyo amesema kuwa hapendi siasa na hata siku ikitokea akapatiwa nafasi ya uongozi hataweza kufanya kwa kuwa maisha yake kitu kinachompatia furaha ni uigizaji.