Jumanne , 21st Nov , 2017

Kundi la wasanii wa muziki wa Tanzania kutoka visiwani Zanzibar, Off Side Trick, wamesababisha kufungwa kwa tamasha la utamaduni la Lamu huko Mombasa nchini Kenya, baada ya kucheza mtindo usiofaa wenye kukiuka maadili.

Taarifa kutoka Mombasa zinasema kwamba kitendo hiko kililalamikiwa na wakazi wa eneo hilo, viongozi wa dini na viongozi wa utamaduni wa Kenya, baada ya kuangalia kile kilichokuwa kikiendelea jukwaani na kulazimu tamasha hilo kufungwa.

Baadhi ya watu walijaribu kuwaonya kundi hilo kuacha kucheza michezo hiyo ya uchafu ambayo sio maadili lakini walijifanya kutosikia, na ndipo waandaaji wa tamasha na viongozi wa eneo hilo kupanda jukwaani na kuwashusha kwa nguvu .

Baada ya tukio hilo Mkurugenzi Msaidizi wa Nyumba ya Maonyesho wa Kenya, Bwana  Athman Hussein, amesema kuna haja ya kuwahakiki wasanii kabla hawajapanda jukwaani, kwani kitendo hiko kimedhalilisha jamii ya hapo na mji wa Lamu kiujumla, kwani mji huo ni maarufu kwa utalii na pia uko chini ya Urithi wa dunia wa UNESCO.