Jumatatu , 5th Oct , 2020

Ikiwa leo dunia inaadhimisha siku ya makazi baadhi ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam wamesema serikali haina budi kuchukua hatua kali kwa watu wanaojenga katika maeneo hatarishi huku wengine wakitoa malalamiko yao juu ya uwepo wa kundi kubwa la matapeli katika sekta ya ardhi.

Ramani ya makazi ya watu

EATV hii leo imepita katika mitaa kadhaa ya Jiji la Dar es Salaam na kuzungumza na wananchi hao ambao wameelezea adha wanayokutana nayo ikiwemo madalali ambao wamekuwa wakipangisha nyumba kwa gharama kubwa, hali ambayo imekuwa inaleta usumbufu kwa muda mrefu.

Pamoja na hayo EATV ikalazimika kufika katika chama cha wapangaji Tanzania na kuzungumza na Katibu wake Bw. Ngasongwa Philip, ambaye amesema ili kuepusha migogoro ya ardhi ni muhimu wadau wote kufuata sheria.

"Sasa unakuta mwenye nyumba anataka alipwe kodi ya mwaka mzima wakati hata waajiri hawalipi mishahara ya mwaka mzima hii ni changamoto kubwa sana". amesema Ngasongwa Philip Katibu wa Chama cha wapangaji, Ngasongwa Philip.

Aidha, amesisitiza kuwa mfumo rasmi wa upangishaji unaotumika kwa kuwa  sasa ni holela hasa katika makazi ambayo hayajapangwa ukiacha machache yaliyokidhi vigezo akishauri katika siku hii ni vyema wadau wakatafakari uwepo wa udalali usio rasmi ambao huumiza wananchi kwa muda mrefu.