Jumanne , 3rd Nov , 2020

Wakati vijana wengine wakioa na kuolewa kumekuwepo na wimbi la vijana wengi ambao wamejawa na hofu, woga juu ya suala zima la ndoa huku moja wapo ya sababu ya hali hiyo ikitajwa kuwa kukithiri kwa matukio ya ukatili miongoni mwa wanandoa.

East Africa Digital imeongea na Mwanasosholojia, Rajabu Mpilipili, kutoka TAYA ambapo amesema matukio ya ukatili baina ya wanandoa yamepelekea vijana wengi kuona ndoa kama kitanzi na kuathiri afya ya akili .

“Vijana wanaathirika kwa namna mbalimbali wengine wanafika hatua hawaoni thamani ya ndoa kwasababu anaona kama kwenye ndoa ukatili unakuwa wa namna hii wa watu kumwagiana maji ya moto, kupigwa,kwa hiyo wanaona bora wabaki kwenye mahusiano ya kawaida" amesema Mpilipili

Aidha Mpilipili ameongeza kuwa athari hii haishii kwenye kuona ndoa kama kitanzi bali huathiri afya ya kaili ya vijana kwa kuwasababishia msongo wa mawazo.

“Afya ya akili inakuwa ina matatizo mmoja kwa mmoja wanajikuta wanakuwa na msongo wa mawazo, wana maswali mengi akilini mwao kuhusina mifumo hii na wanakuwa wanashindwa namna gani waweze kuyajibu kwani pale ambapo ungetegemea kupata majibu sahihi kwa wahusika lakini wahusika haohao ndio wanaokithirisha hivyo vitendo” amesema Mpilipili