Jumatatu , 25th Oct , 2021

Meneja wa Barcelona Ronald Koeman amezidi kukalia kuti kavu ndani ya miamba ya Catalan baada ya kupokea kichapo cha magoli 2-1 kutoka kwa Real Madrid nyumbani katika uwanja wa Camp Nou.

Kocha wa Barcelona, Ronald Koeman akifuatilia kwa umakini mchezo wa timu yake.

Kichapo hicho kilipelekea mashabiki wa Barcelona baada ya mchezo kumalizika kulizuia gari aliyokuwamo kocha Koeman kuondoka kwenye uwanja wa Camp Nou.

Kupitia ukurasa wa twitter wa Barca umeandika "FC Barcelona inapinga vikali vitendo vya vurugu na dharau alivyofanyiwa kocha wetu akiwa anaondoka uwanjani ,klabu itachukua hatua kali za kinidhamu na za kiusalama ili matukio kama hayo yasiweze kujitokeze siku nyingine”

Huu unakuwa El Classico ya kwanza baada ya miaka 16 kutohusisha wachezaji Lionel Messi na Sergio Ramos tangu mwaka 2005 huku kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 65 wachezaji sita vijana wakianza kati ya wachezaji 22 huku kiungo wa fc Barcelona Gavi 17,akiweka rekodi ya karne ya mchezaji kinda kuanza kwenye mchezo wa El classico.

Hiki kinakuwa kichapo cha nne mfululizo kwa Barcelona kwenye El Clasico tangu mwaka 1965 na sasa kusalia nafasi ya tisa kwenye la liga na kuwa nyuma ya alama 5 dhidi ya Real Madrid.